Friday, August 3, 2012

Mahakama yapiga ‘stop’ mgomo wa walimu



Rais wa Chama cha Walimu Tanania (CWT), Gratian Mukoba akiwa ameambatana na baadhi ya walimu wakati wakitoka Mahakama kuu, kitengo cha kazi jijini Dar es Salaam jana kusikiliza maamuzi ya mahakama hiyo kuhusu kesi yao dhidi ya Serikali. Mahakamama ilisitisha mgomo wa walimu ikidaiwa kuwa ni batili. Picha na Venance NestoryMAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Kazi imesitisha mgomo wa walimu na kuwataka kurudi kazini mara moja.
Mahakama hiyo pia imeuagiza uongozi wa Chama cha Walimu (CWT) kuandaa taarifa kwa umma, kutangaza kusitishwa kwa mgomo huo kama walivyowatangazia wanachama wake wakati ulipoanza.

Mahakama hiyo ilisitisha mgomo huo jana wakati ilipotoa uamuzi wa maombi yaliyowasilishwa mahakamani na Serikali. Jaji Sophia Wambura aliyekuwa akisikiliza maombi hayo, alisema mgomo huo ni batili kwa kuwa haukukidhi masharti ya Sheria ya Ajira na Uhusiano Kazini.

Katika uamuzi wake, mahakama hiyo pia imekitaka CWT kulipa hasara za kifedha au kuwafidia wanafunzi vipindi vya masomo walivyovikosa, hususan wale wa darasa la saba. Mahakama hiyo ilikwenda mbali zaidi na kuwaonya walimu na Serikali kwa kitendo cha kuzungumzia suala hilo wakati tayari lilikuwa mahakamani.

Jaji Wambura alisema kitendo hicho ni uvunjaji wa Ibara ya 4 na ya 107 A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 kama ilivyokwisha kurekebishwa mara kadhaa.

“Vinginevyo, hakukuwa na haja ya kuja hapa mahakamani kabisa. Kama kila mmoja ataachwa awe jaji, itakuwa ni kero na uvunjaji wa utawala wa sheria,” alisema Jaji Wambura.

Jaji huyo alizitaka pande zote kurudi kwenye meza ya mazungumzo na kushauri kuwa, ikiwezekana zialike watu wenye ujuzi wa masuala ya sheria za kazi na uhusiano kazini kuwasaidia ili kufikia makubaliano kwa amani.

“Chini ya Masharti ya Kifungu cha 81 (1) (2) cha Sheria ya Ajira na Uhusiano Kazini, natamka kuwa mgomo ambao umekuwa ukiendelea kwa siku tatu sasa ni kinyume cha sheria. Ninaamuru usitishwe na walimu wote warudi kazini mara moja,” aliagiza Jaji Wambura.

Msingi wa uamuzi
Jaji Wambura alirejea hoja zilizowasilishwa na pande zote, waombaji wakiwakilishwa na Mawakili wa Serikali Wakuu, Obadia Kameya na Pius Mboya na wajibu maombi (CWT) wakiwakilishwa na Wakili Gabriel Mnyele.

Alisema baada ya kupitia hoja zote na vielelezo vilivyoambatanishwa kwenye hati za viapo pamoja na majibu husika, amebaini kuwa na kuridhika kuwa mgomo huo haukufuata sheria.

Alisema CWT hawakufuata masharti ya kifungu cha 80 (1), cha Sheria ya Ajira na Uhusiano Kazini na kwamba kulikuwa na dosari kwani kura zilizopigwa zilipotosha wanachama , kwa sababu hazikuwa za kuunga mkono mgomo, bali madai ya walimu.

Jaji huyo alisema upigaji kura ulikuwa ni batili kwani walimu hawakufahamishwa matokeo ya mgomo huo na kwamba haukuzingatia taratibu.

Pia alisema taarifa ya mgomo iliyowasilishwa kwa Katibu Mkuu Kiongozi Julai 27, 2012 saa 9:00 alasiri wakati mchakato wa upigaji kura ukiwa unaendelea, pia ilikuwa ni batili.

Dosari nyingine ni kutoeleza kikomo cha mgomo na kutokubainisha kama watawalipa wanachama wake wakati wa mgomo.

Aliongeza kwamba, CWT kwa kushindwa kutimiza masharti ya kanuni ya 42 na 43 za sheria husika, kulisababisha kero zisizo za lazima.

Alisisitiza kuwa kitendo cha CWT kuwasilisha taarifa ya mgomo Ijumaa saa 9:00 wakidai mgomo unaanza Jumatatu, hali wakijua kuwa Jumamosi na Jumapili hazikuwa siku za kazi, ni kinyume cha kanuni na kilifanywa kwa nia mbaya.

Wakili wa CWT, Mnyele alisema anasubiri maelekezo ya wateja wake, lakini Rais wa CWT, Gratian Mukoba alisema watatoa tamko leo.

Mgomo waendelea
Katika baadhi ya shule za Dar es Salaam jana mgomo uliendelea na kusababisha wanafunzi kadhaa kuonekana wakizurura mitaani.

Shule hizo zimo za sekondari na msingi ambazo ni Mchangani, Mwananyamala Kisiwani, Kunduchi, Pius Msekwa, Pwazo, Pwani, Mtakuja, Mtongani na Kisauke katika manispaa ya Kinondoni.

Walimu walioonekana maeneo ya shule hizo walikuwa wachache huku wanafunzi nao wakionekana wakisambaa hovyo katika maeneo ya shule.

Baadhi ya wanafunzi walikiri kwamba mahudhurio yao pia yamezorota.

Mwalimu Mkuu Msaizi wa Shule ya Msingi Mwananyamala Kisiwani, Abwalib Mfinanga alisema; “Kama unavyoona, walimu hawaingii madarasani kufundisha kutokana na mgomo unao endelea.”

Katika Manispaa ya Temeke baadhi ya wanafunzi wa darasa la saba walisikika wakilalamika kutotendewa haki.

“Walimu wetu wamesoma na sisi tunataka tuwe kama wao, tunawaomba watufundishe ili tuweze kufikia kiwango kama chao,” alisema mwalimu Alfred Mwinuka.

Katika shule ya Msingi Amani wanafunzi walionekana wakicheza katika viwanja vya michezo na wakati katika shule ya Msingi ya Dovya, baadhi ya madarasa yalikuwa yamefungwa huku baadhi ya wanafunzi wakiwa wamezagaa nje.

Mwanafunzi Saleh Juma alisema kuwa jana ni mwalimu mmoja tu aliyeingia darasani, na baada ya muda mfupi aliondoka. Mwalimu Mkuu peke yake ndio tunamuona akipita madarasani,” alisema Saleh.

Wachangishana fedha
Wazazi wa wanafunzi wa darasa la saba katika shule ya msingi Manzese, Dar es Salaam wamekubali kuingia gharama kwa kuwalipa walimu ili wawafundishe watoto wao ambao wanakabiliwa na mitihani Taifa Septemba 12, mwaka huu.

Wakizungumza na Mwananchi kwa nyakati tofauti, wazazi hao walidai kuwa katika mkutano uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita, walikubaliana kila mtoto alipe Sh15, 000 ili walimu waweze kuwafundisha hadi mitihani yao ya Taifa itakapokuwa inakaribia.

Mwalimu Mkuu Msaidizi, Rehema Abdallah alikiri kuwepo kwa utaratibu huo ambao alisema kuwa uliridhiwa katika kikao cha wazazi na kamati ya shule hiyo uliofanyika wiki iliyopita.

Mwalimu huyo msaidizi alibainisha kuwa mpango huo wa masomo umelenga wakati shule zitakuwa zimefungwa.

HakiElimu wanena

Mkurugenzi wa Shirika la Haki Elimu, Elizabeth Missokia ameitaka Serikali kutatua madai ya walimu haraka ili wanafunzi wasiendelee kuathirika.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Missokia alisema utafiti uliofanywa na Shirika hilo mwaka jana, ulibaini kuwa, kwa muda mrefu walimu wamekuwa katika mgomo baridi.

“Utafiti tuliofanya umebaini kuwa asilimia 40.6 ya walimu katika sampuli ya utafiti ndio walioonyesha nia ya kuendelea na kazi hiyo,” alisema na kuongeza:

“Hilo limesababishwa na mazingira magumu ya kufanyia kazi na ufinyu wa maslahi.”

Missokia aliongeza: “Tunaweza kuthibitisha hilo hata kwa kuangalia kiwango cha elimu takribani miaka mitatu iliyopita.”

Wampinga JK
Shirikisho la Vyama Vya Wafanyakazi (Tucta) limesikitishwa na hotuba ya Rais Jakaya Kikwete ya kudai kuwa Serikali haina uwezo wa kuwalipa walimu.

Katibu Mkuu wa Tucta, Nicolaus Mgaya aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kitendo cha Serikali cha kudai kwamba haina fedha za kuwalipa walimu ni ishara tosha ya kuwa, haiwajali walimu.

Alisema kauli hiyo inazidi kuwavunja moyo na kuwafanya washindwe kufanya kazi kwa moyo.

“Si kweli kwamba Serikali haina fedha za kuwalipa walimu. Fedha zipo, Ila hawajaamua kuwalipa,” alisema Mgaya.