Thursday, September 19, 2013

Padri aliyemwagiwa tindikali kusafirishwa nje kwa matibabu


Paroko wa Parokia ya Roho Mtakatifu Cheju Zanzibar, akisaidiwa na Frateri, Richard Haki kupumzika kitandani baada ya kuzungumza na waandishi katika katika Wodi ya Kibasila iliyopo katika Hosipitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) jijni Dar es Salaam .

Huenda Padri wa Kanisa Katoliki Parokia ya Mpendae Zanzibar, Anselmo Mwang’amba aliyemwagiwa tindikali siku tano zilizopita, akasafirishwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu kutokana na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ambako amelazwa, kudaiwa kushindwa kumtibu.

Akizungumza jana, padri huyo alisema anategemea kwenda nje ya nchi kwa matibabu japokuwa bado hajajua nchi atakayopelekwa kwa kuwa anasubiri ushauri wa madaktari.

Alisema pamoja na matibabu aliyoyapata lakini bado anasikia maumivu katika majeraha ya usoni, mikononi na kifuani.

Aliisihi Serikali kukomesha na kuwakamata wahusika wa vitendo hivyo vilivyokithiri vya kuwamwagiwa watu tindikali bila sababu visiwani humo.

Hata hivyo, habari zilizopatikana kutoka katika chanzo kilichopo ndani ya hospitali hiyo kimeeleza kuwa, padri huyo anatarajia kupelekwa nje ya nchi kwa matibabu kwani inadaiwa majeraha yake yameshindikana kutibiwa nchini, japokuwa bado haijajulikana ni nchi gani atakayoenda kati ya mbili zinazotajwa na viongozi hao, Afrika Kusini na India.

Alisema madaktari wataalamu waliopo katika hospitali hiyo wana uwezo wa kumponya Padri huyo lakini tatizo lililopo ni ukosefu wa vifaa vya kisasa ndiyo maana wagonjwa wengi wanaomwagiwa tindikali hupelekwa kutibiwa nje ya nchi.