Friday, May 24, 2013

Gesi Mtwara isiigawe Tanzania

 
Huenda ni bahati mbaya kwamba mgawanyo usiyo sahihi au sawa kwa rasilimali hizi, ulafi wa baadhi ya viongozi, hasa wale waliokabidhiwa jukumu la kusimamia idara au taasisi zinazoshughulikia uchimbaji, usambazaji wake na usiri mkubwa katika mikataba.
 

 Dar es Salaam. Bara la Afrika kwa hakika limebarikiwa kuwa na rasilimali lukuki ambazo ni lulu katika kukuza uchumi.

Licha ya utajiri huo mkubwa unaweza kujiuliza, je, ni kwanini bara hili limeendelea kuwa maskini kwa miaka mingi huku likikabiliwa na mizozo mingi na migogoro kuhusu mgawanyiko wa rasilimali hizi.

Jiulize, leo ikiwa ni miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU), sasa Umoja wa Afrika (AU), kwanini bara hili tajiri kiasi hiki bado linatajwa kuwa maskini pengine kuliko mabara mengine duniani?

Tunaambiwa, Afrika ina asilimia kubwa ya madini, lakini, jiulize, kwa nini asilimia kubwa ya madini hayo haitumiwi vizuri au kikamilifu katika kuliinua bara hili. Kwanini hayalisaidii bara hili?


Kwa kutaja machache, Afrika ni tajiri kwa madini kama vile, almasi, dhahabu, shaba urani na mengine mengi.


Bara hilo linajivunia asilimia 40 ya umeme wa nguvu za maji unaopatikana duniani, linazalisha madini mengine kama chromium, asilimia 30 ya uranium na asilimia 50 ya dhahabu inayopatikana kote duniani.

Pia, asilimia 90 ya cobalt, asilimia 50 ya phosphates, asilimia 40 platinum, asilimia 7.5 au zaidi ya makaa ya mawe, asilimia 8 ya petroli na bidhaa zake, asilimia 12 ya gesi asilia, asilimia 3 ya madini ya chuma na mamilioni ya ekari za ardhi nzuri na inayofaa kwa kilimo cha mazao mbalimbali yakiwamo ya chakula, biashara ambayo ni mengi mno kuyataja.

Pia, bara hili linayo mito, maziwa, bahari ambako kwa kiasi kikubwa wanapatikana samaki wengi na wa aina mbalimbali wakiwamo hata wale wenye bei kubwa katika soko la dunia.

Pia, Afrika inavyo vitu vingine vingi kama mbuga za wanyama ambazo zimejaa tele, zinavutia watalii wengi, ambao huongeza fedha za kigeni, lakini mbona havijaweza kulisaidia bara hili kuondokana na lindi hili la umaskini?


Huenda ni bahati mbaya kwamba mgawanyo usiyo sahihi au sawa kwa rasilimali hizi, ulafi wa baadhi ya viongozi, hasa wale waliokabidhiwa jukumu la kusimamia idara au taasisi zinazoshughulikia uchimbaji, usambazaji wake na usiri mkubwa katika mikataba.
 

Kutokana na usimamizi duni wa rasilimali hizi zinaweza kuwa baadhi ya sababu za kuzuka kwa mizozo hii mikubwa ambayo inalikumba bara hili, kama ambavyo inaanza kuzuka Tanzania.

Rais Yoweri Museveni wa Uganda katika moja ya hotuba zake mwaka jana wakati akizindua mradi wa kuchimba mafuta katika Ziwa Natron nchini mwake alieleza mengi kuhusu rasilimali hizi na jinsi zinavyoweza kuigawa nchi na Afrika kwa jumla.