Thursday, August 30, 2012

Chadema ‘yakomalia’ kifo cha Morogoro


CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema hakina imani na Tume iliyoundwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) kuchunguza mauaji yanayodaiwa kufanywa na Polisi mkoani Morogoro wakati wa maandamano ya chama hicho.

Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika alisema hayo jana Dar es Salaam wakati akitoa taarifa juu ya tukio la mauaji ya muuza magazeti wa eneo la Msamvu, Ally Zona (38).

Alisema kuna mgongano wa taarifa kuhusu tukio hilo kutoka kwa mashahidi na Polisi, akidai kuwa kifo hicho kina utata na hakiwezi kuchunguzwa na Polisi.

“Kiundwe chombo kingine huru cha uchunguzi au Rais Kikwete (Jakaya) aingilie kati iundwe Tume huru kuchunguza kifo hiki, kwani hii ya sasa haiwezi kuchunguzwa na polisi kwani wao ni watuhumiwa,” alisema Mnyika na kuongeza kuwa hata baadhi ya viongozi wa chama chake ni mashahidi.

Aidha, alisema chama hicho kwa kuheshimu sheria, kimeamua kusitisha operesheni ya vuguvugu ya mabadiliko iliyokuwa iendelee Iringa, na kuomba maelezo kutoka kwa Serikali na Polisi kuwa ni kwa nini vyama vingine vinaendeleza matukio ya kisiasa yenye halaiki ya wananchi huku Polisi wakiinyima Chadema ruhusa ya kufanya hivyo.

“Kwa mfano, Lindi Mjini kuna maandamano ya wafuasi wa CCM wanarudisha fomu kuwania nafasi za uchaguzi, huku polisi mikoani wakisema mikutano inayofanyika sasa inaingilia ratiba ya sensa,” alihoji Mnyika.

Alisema kutokana na tukio la Morogoro ipo haja ya sheria ya vifo vyenye utata ianze kutumika sasa ili kupata Tume huru ambayo itashughulikia mgogoro wa Morogoro na kuupatia suluhu stahiki.

Kuhusu kusaidia matibabu ya majeruhi wa tukio hilo, Mnyika alisema chama hicho kitahakikisha kinatoa matibabu yao na kuwezesha maziko ya marehemu huyo.

Hata hivyo, hakuzungumzia sababu ya kufanya maandamano juzi huku sensa ikiendelea na kuja kushituka baadaye na kusitisha operesheni yao.