Wednesday, July 11, 2012

Usajili wa madaktari 390 wasitishwa

BARAZA la Madaktari Tanganyika limesema madaktari 390 waliokuwa mafunzoni katika hospitali mbalimbali nchini na kugoma kazi, wamepoteza sifa na kwa sababu hiyo, usajili wao umesitishwa.

Kutokana na hali hiyo, usajili wao wa muda umesitishwa kuanzia leo na madaktari wote wanaohusika, wametakiwa kurejesha hati za usajili wa muda kwenye Ofisi ya Msajili wa Madaktari kabla ya Julai 17.
Hatua hiyo imo katika taarifa kwa umma iliyotolewa jana na Mwenyekiti wa Baraza la Madaktari Tanganyika, Dk Donan Mmbando.
Taarifa ya Dk Mmbando ilieleza kwamba imechukua hatua hiyo baada ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, kumwandikia akilalamikia hatua ya madaktari hao kugoma.
Kwa mujibu wa Dk Mmbando, Katibu Mkuu Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii aliwasilisha malalamiko kwenye Baraza la Madaktari Tanganyika kwamba madaktari waliogoma walikataa kutoa huduma za kitaalamu, ikiwa ni wajibu wao na kwamba kitendo hicho kilihatarisha maisha ya wagonjwa katika hospitali husika na pia ni kinyume cha maadili ya taaluma ya udaktari.
Mwenyekiti huyo alieleza, kwamba walipokea malalamiko kutoka kwa Katibu Mkuu, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, kwamba baadhi ya madaktari waliopata usajili wa muda ili kuwawezesha kufanya mafunzo kwa vitendo, waligoma kutoa huduma kwa wagonjwa kati ya Juni 23 na 29.
Ilieleza kuwa madaktari hao walipangiwa kutoa huduma kwa wagonjwa katika hospitali za Muhimbili, K.C.M.C, Rufaa Mbeya, Bugando, Amana, Temeke, St. Francis- Ifakara, Mwananyamala, Sekou Toure, Hydom na Dodoma.
“Kutokana na malalamiko hayo, Msajili wa Baraza la Madaktari Tanganyika, alimwandikia kila daktari aliyelalamikiwa Taarifa ya Kusudio la Kufanya Uchunguzi dhidi yake, juu ya malalamiko yaliyowasilishwa na Katibu Mkuu, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.
“Baraza la Madaktari Tanganyika limebaini kuwa, kwa mujibu wa kifungu cha 15(2) cha Sheria ya Madaktari, Sura ya 152, madaktari waliokuwa kwenye mgomo na ambao kwa sasa wameondolewa katika hospitali walizokuwa wakifanya mafunzo kwa vitendo, wamepoteza sifa za usajili wa muda,” ilieleza taarifa ya Dk Mmbando.
“Kwa kuzingatia masharti ya sheria kuhusu kupata usajili wa muda, Baraza la Madaktari Tanganyika limeridhika, kwamba madaktari wote ambao majina yao yameorodheshwa katika taarifa hii, wamepoteza sifa na kwa sababu hiyo, usajili wao umesitishwa kuanzia Julai 11,” ilisema taarifa.
Alitaja idadi ya madaktari 390 na hospitali walizotoka kuwa ni Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (103); KCMC (66); Rufaa Mbeya (55); Rufaa Bugando (43); Amana (26); Temeke (17), St Francis (17); Mwananyamala (26); Sekou Toure (14), Hydom (14) na Dodoma (2).
Madaktari hao waligoma baada ya kushindwa kuafikiana na Serikali katika nyongeza ya mshahara ambao walikuwa wakitaka walipwe Sh milioni 3.5 kwa daktari anayeanza kazi ambaye ikijumuishwa na posho nyingine, atakuwa na mshahara wa Sh milioni 7.7.
Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi uliopita, aliwaeleza madaktari hao kwamba Serikali haina uwezo wa kulipa kiwango hicho, na wako huru kutafuta mwajiri mwingine anayeweza kuwalipa na hivyo hawana sababu ya kugoma.