WABUNGE vijana wa bunge la Tanzania
wataanza kushiriki mafunzo maalum ya Jeshi la Kujenga Taifa(JKT) ya
miezi mitatu sambamba na mafunzo ya vijana kwa mujibu wa Sheria mwaka
ujao.
Akiwasilisha bungeni hotuba ya Wizara ya
Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Waziri wa wizara hiyo Shamsi Vuai
Nahodha alisema wabunge hao vijana wataungana na kundi la kwanza la
vijana 5000 katika mafunzo hayo yaliyopangwa kuanza i Machi 2013.
Waziri Nahodha alisema bungeni kuwa,
wakati wa mjadala wa bajeti ya Wizara hiyo ya mwaka 2011/2012 wabunge
hao waliomba kupata mafunzo hayo.
“ Ni imani yetu kuwa pamoja na
waheshimwa wabunge kunufaika na mafunzo hayo watahamasisha zoezi la
urejeshwaji wa mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria na kutoa taswira
nzuri ya mafunzo hayo kwa jamii. Naomba waheshimiwa wabunge mjiorodheshe
kwa maandalizi ya mafunzo haya,” amesema Nahodha.
Amesema, ingawa JKT lipo tayari kuchukua
vijana 20,000 kwa wakati mmoja haitaweza kufanya hivyo kutokana na
gharama za kuendeshea mafunzo hayo kuwa kubwa.
“Vijana hao ni miongoni mwa vijana
41,348 ambao watahitimu mafunzo ya Kidato cha Sita katika mwaka 2013.
Kwa hivyo, Wizara imeweka vigezo maalumu vya kuwapata vijana hao kwa
kuzingatia makundi. Makundi ya vijana hao yatatangazwa mwezi Januari
2013,” amesema.
Nahodha amesema, mafunzo hayo ya vijana
kwa mujibu wa sheria yatafanyika kwa miezi sita katika kambi za
Bulombora na Kanembwa (Kigoma), Mlale (Ruvuma), Mafinga (Iringa), Msange
(Tabora) na Oljoro (Arusha).
Akizungumzia umuhimu wa matrekta katika
kuendeleza Kilimo Kwanza, alisema Serikali imepunguza bei ya matrekta
katika Shirika la SUMA-JKT ambapo matrekta yenye “horse power” 50
yaliyokuwa yakiuzwa shilingi milioni 25.6 sasa yanauzwa shilingi milioni
16.5 na matrekta yenye “horse power” 70 yaliyokuwa yanauzwa shilingi
milioni 45.8 sasa yanauzwa shilingi milioni 38.8.
“Hivi sasa Shirika linawapunguzia wateja
malipo ya awali (down payment) kutoka asilimia 50 ya bei ya trekta moja
hadi asilimia 30. Vile vile Shirika linafikiria kupunguza zaidi malipo
ya awali hadi asilimia 15 kwa wateja watakaonunua matrekta kuanzia 50 na
kuendelea. Halikadhilika, Halmashauri za Wilaya ambazo zitakuwa tayari
kuwadhamini wakulima wadogo wadogo imependekezwa zilipe malipo ya awali
ya asilimia 10,” alisema.
Aidha alisema hadi kufikia tarehe 09
Julai, 2012 SUMAJKT ilikuwa imeuza matrekta 786 na kwamba katika
kusogeza matrekta karibu na wateja wake, SUMAJKT imefungua vituo vya
kuuzia matrekta hayo katika mikoa ya Dodoma, Mbeya, Mwanza na Arusha.
“Nimemwagiza wakala wa uuzaji wa
matrekta kufanya mipango ya kuyahamishia matrekta yaliopo Mwenge Dar es
Salaam na kuyapeleka Morogoro. Shirika la SUMAJKT linatarajia kufungua
vituo zaidi vya mauzo ya matrekta kupitia kwa Wakuu wa Mikoa ili
kurahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali kama vile ushauri na
vipuri, alisisitiza.
Kuhusu kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa
suala la migogoro ya ardhi ina ya jeshi na wanachi alisema Wizara
imeanza kuchukua hatua mbalimbali.
“Katika baadhi ya maeneo tutalazimika
kuwaondoa wavamizi mara moja ili kupisha shughuli za jeshi. Aidha, kwa
maeneo ambayo uingiaji wa watu umezidi kiwango kiasi cha kufanya eneo
husika kutokufaa tena kwa shughuli za Jeshi, tutashauriana na mamlaka
zinazohusika kuangalia uwezekano wa kupewa maeneo mbadala,” Waziri
Nahodha alisema.
Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga
Taifa imeliomba kuidhinisha jumla ya shilingi 1,086,550,058,000.00
ambazo kati yake shilingi 678,363,492,000.00 zitatumika kwa ajili ya
bajeti ya matumizi ya kawaida na shilingi 408,186,566,000.00 ni bajeti
ya matumizi ya maendeleo.